TAASISI ZA BIMA ZITOE ELIMU KWA WANANCHI KUHUSU UMUHIMU WA KUKATA BIMA
Muhtasari: Taasisi za Bima nchini zimeshauriwa kutoa elimu
kuhusu umuhimu wa kukata bima kwenye shughuli wanazofanya kwa wananchi ambao inadaiwa wengi wao hawana
uelewa wa huduma zinazotolewa na taasisi hizo.
Na Mwandishi Wetu, Dodoma
MAMLAKA ya usimamizi wa bima nchini (TIRA) kwa
kushirikiana na wadau wa bima wameshauriwa kutoa elimu ya bima kwa wananchi
hasa yanapotokea majanga kwa wateja wao ili wananchi wengi wajue umuhimu wa
kukatia bima shughuli zao za uchumi.
Ushauri huo umetolewa leo ijumaa, Septemba 13, 2024 na Mkuu wa
Wilaya ya Chamwino, kwenye matembezi ya kuadhimisha siku ya bima nchini
yaliyofanyika kwenye viwanja vya Nyerere Square Jijini Dodoma.
Mayanja amesema ni Watanzania wachache wenye uelewa kuhusu
huduma za bima na kundi kubwa halina elimu hivyo yanapotokea majanga kwa wateja
wao wenye bima basi watumie fursa hiyo kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu
wa kuwa na bima.
“Nina fahamu Tira mnafanya kazi kubwa kwa kushirikiana na wadau
wa sekta binafsi lakini ukiangalia namna nchi yetu na wananchi wake wanavyopiga
hatua za kimaendeleo kwa kujishughulisha na shughuli mbalimbali za kiuchumi bado
kuna changamoto za wadau kukatia bima shughuli wanazozifanya japo tumeona ni
kwa jinsi gani bima imeweza kujerejesha kile ambacho kimepotea,” amesema
Mayanja
Amezitaka taasisi za bima nchini ziwe na mipango madhubuti ya
kuhakikisha Watanzania walio wengi wanapata elimu ya bima ambapo wakipata elimu
ya kutosha kwa fursa zilizopo watachukua hatua maana wenye uelewa wa bima ni
wale tu ambao wapo kwenye nafasi mbalimbali za utumishi au wafanyabiashara
wakubwa huku kundi kubwa la wananchi wakiachwa nyuma.
“Lakini kuna kundi kubwa sana ambao hawafahamu wala hawana
uelewa mkubwa juu ya bidhaa za bima mlizonazo kwa hiyo niwaombe tuongeze nguvu
katika eneo hilo ili tuwe na maendeleo ya pamoja,” amesema Mayanja na kuongeza
kuwa.
“Najua yanapotokea majanga mbalimbali mmekuwa mkirejesha mitaji
ya shughuli zile ambazo zimepotea basi ikitokea wakati huo fanyeni promo ya
kutosha ili watanzania wajue ya kwamba yanawezekana kwa sababu msipofanya hivyo
wataona ni mambo ya kawaida.”
Kwa upande wake Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya kati, Janeth Shango
amewataka Watanzania kukatia shughuli zao za kiuchumi bima ili yanapotokea
majanga wasitetereke bali waweze kuinuka na kuendelea na mapambano kwa sababu
bima inawasaidia wafanyabiashara kurejesha mitaji yao hata baada ya kupata
majanga.
“Tunaona mara nyingi masoko yanashika moto na kuteketeza mali
zote lakini kama umekatia biashara yako bima baada ya muda unarudi kuendelea na
biashara yako tofauti na yule asiye na bima ambapo hupoteza kila kitu na
kulazimika kuanza upya,” amesema Shango.
Aidha taasisi hizo za bima nchini zimetoa msaada wa kuchangia
damu kwenye kituo cha damu salama kilichopo mkoa wa Dodoma na msaada wa vifaa
tiba vyenye thamani ya Sh15 milioni kwenye
wodi ya watoto njiti iliyopo hospitali ya rufaa ya mkoa wa Dodoma.
Mwisho….


Comments
Post a Comment