TMDA YATOA MSAADA WA DAWA NA VIFAA TIBA VYENYE THAMANI YA SH 24 MILIONI

 

Muhtasari: Mamlaka ya dawa na vifaa tiba (TMDA) Kanda ya kati imetoa msaada wa vifaa tiba, dawa na vitendanishi vyenye thamani ya Sh24 milion kwenye gereza kuu la Isanga lililoko Mkoani Dodoma kwa ajili ya kuwahudumia wafungwa, mahabusu na askari magereza wapatao 1,489.


Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

WAMILIKI wa maduka ya dawa nchini wametakiwa kufuata masharti ya leseni zao za kufanya biashara hiyo ili wasihatarishe afya za watumiaji.

Kauli hiyo imetolewa leo jumanne Juni 18, 2024 na Meneja wa Mamlaka ya dawa na vifaa tiba (TMDA) kanda ya kati, Sonia Mkumbwa wakati akitoa msaada wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi vyenye thamani ya Sh24 milion kwenye gereza kuu la Isanga lililopo Mkoani Dodoma.

Mkumbwa amesema dawa hizo zimepatikana kwenye msako unaofanywa na mamlaka hiyo kwenye maduka ya dawa na vitendanishi ambavyo vimekuwa vikihifadhiwa kwenye maeneo ambayo hayapaswi kuhifadhiwa.


Meneja wa mamlaka ya dawa na vifaa tiba (TMDA) Kanda ya kati, Sonia Mkumbwa (wa tano kulia) akimkabidhi msaada wa dawa na vifaa tiba mkuu wa gereza la Isanga lililopo Jijini Dodoma, Zefania Neligwa (wa tatu kushoto

Amesema zipo taratibu na masharti ya kuhifadhi dawa hizo hivyo ni lazima wanaotoa huduma za dawa za binadamu kuzifuata ili dawa ziendelee kuwa kwenye hali nzuri bila kuleta madhara kwa binadamu.

“Kikawaida  kila dawa ina mazingira yake ya kuhifadhiwa na dawa nyingi zinatakiwa kuhifadhiwa kwenye nyuzi joto lisilozidi 30 na nyingine zinatakiwa kuhifadhiwa kwenye majokofu lakini dawa hizo zilikutwa zimehifadhiwa kwenye mazingira ambayo siyo salama na kama zingeachwa zingeweza kuleta madhara kwa mtumiaji,” amesema Mkumbwa na kuongeza kuwa

“Kuna dawa nyingine tumezikuta kwenye maduka ya dawa lakini maduka hayo hayana wataalam wa kuzitumia dawa hizo hivyo kuleta hatari kwa watumiaji kwa sababu hakuna mtaalam wa kuwaelekeza matumizi ya dawa hizo hivyo ni lazima wafuate masharti ya leseni zao ili wasihatarishe maisha ya wagonjwa.”

Dawa ambazo zimepelekwa kwenye gereza hilo ni pamoja na dawa za kupunguza maumivu, anti bayotiki dawa za shinikizo la damu na zingine za vidonda ambapo meneja huyo amesema dawa hizo bado zipo kwenye hali nzuri kwa ajili ya matumizi ya binadamu na hivyo zinaweza kutumika bila shida yoyote.



Mkuu wa gereza la Isanga, Zefania Neligwa amesema msaada huo umekuja kwa wakati kwani gereza hilo linapokea watu wenye matatizo mbalimbali ya kiafya huku wengine wakija na majeraha makubwa yanayohitaji matibabu ya kina.

Amesema hadi leo gereza hilo lina jumla ya wafungwa 1,147 na askari magereza 343  pamoja na familia zao ambao wote wanategemea huduma za matibabu kutoka kwenye zahanati iliyopo kwenye gereza hilo hivyo msaaada huo umekuja kwa wakati.






Naye daktari wa zahanati iliyopo kwenye gereza hilo, Pantaleo Maumba amesema dawa hizo ni msaada mkubwa kwani zahanati hiyo inatibu kundi kubwa la mahabusu na wafungwa ambao wanategemea zahanati hiyo kwa matibabu.

Amesema msaada huo utatumika kama ulivyokusudiwa na kuitaka mamlaka hiyo kuendelea kutoa msaada wa vifaa tiba na dawa kwani mahitaji ni makubwa kulingana na kundi wanalolihudumia.

Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

CHODAWU YAITAKA SERIKALI KURIDHIA MKATABA NAMBA 189 WA WAFANYAKAZI WA MAJUMBANI

NGOs ZAPEWA MWONGOZO WA KULIPA KODI NA TRA