MAJALIWA ATOA MAAGIZO MANNE KWA WIZARA YA KILIMO NA WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI ILI KUKUZA SEKTA HIYO
Muhtasari:
Maonyesho ya kilimo, ufugaji na uvuvi nanenane yamezinduliwa leo Jijini Dodoma
katika viwanja vya Nzuguni ambapo Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa maagizo
manne kwa wizara za kilimo, mifugo na uvuvi, benki ya kilimo (TADB) na maofisa
ugani kuwafikia wakulima na kuwasaidia kutafuta masoko ya bidhaa zao.
Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Dodoma. Waziri
Mkuu Kassim Majaliwa amefungua maonyesho ya kilimo, mifugo na uvuvi maarufu
nanenane na kuziagiza Wizara za kilimo, mifugo na uvuvi kuendelea kusimamia
uhifadhi na utunzaji wa mazingira ambayo yatawawezesha kufanya shughuli za
kilimo, mifugo pamoja na uvuvi katika eneo la uwanja huo kwa kipindi kirefu.
Waziri Mkuu
ametoa kauli hiyo leo alhamisi Agosti 1, 2024 wakati akifungua maonyesho ya kilimo,
mifugo na uvuvi kwenye uwanja wa nanenane yanayofanyika kitaifa Nzuguni Jijini
Dodoma.
Amesema
wakiharibu mazingira kwenye maeneo hayo hawatalima kwa sababu hawatapata maji
ya umwagiliaji, mito na maziwa itakauka na kuagiza suala la utunzaji wa
mazingira liwe ni ajenda ya kudumu kwenye wizara hizo na iende kwenye makundi
yote ya kilimo, mifugo na uvuvi na vyama vya ushirika.
Amezitaka
Wizara hizo pia kuimarisha sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi ili wafugaji
wabadilishe muundo wao wa ufugaji na wavuvi wavue kwa teknolojia mpya lakini
wapate mazao mengi.
“Natambua
zuio mliloliweka ziwa Tanganyika kwa kutovua kwa nyakati ambapo tunaona linakwenda
kuishiashia nadhani mwisho mwezi huu mlizuia kwa miezi mitatu ili wananchi
wasivue kwa wakati huo kwa lengo la kutaka samaki wazaliane ili watakapoanza
kuvua wapate samaki wengi wenye ukubwa utakaoweza kutupatia fedha,” amesema
Waziri Mkuu.
Pia
ameiagiza benki ya maendeleo ya kilimo (TADB )iweke mkakati mahususi ya
kuwafikia wananchi wajue benki hiyo iko wapi na pale ambako hakuna benki
wakulima watawapataje kwa sababu wakulima hao wanahitaji huduma kule walipo
wasigharamie kulipa nauli kwenda umbali mrefu kutafuta benki.
“Hebu
jipangeni wafikieni wakulima, wafugaji na wavuvi na kwenye banda lenu hapa
fanyeni kazi ya kuwaelimisha na kuwahabarisha wapi mlipo na mikopo
inapatikanaje tunatamani kuona watanzania wengi wakiingia kwenye kilimo ambacho
leo kimethibitisha kwamba ndiyo mkombozi wa maisha yetu na uchumi wetu,”
amesema Waziri Mkuu Majaliwa.
Amewaagiza
maofisa ugani popote walipo watumie mifumo ya kidigitali kuwafikia wakulima
wawaambie namna nzuri ya kulima na kufuga na kuvua, namna nzuri ya kutunza
mazao yao lakini pia namna ya kupata masoko kwa sababu hiyo ndiyo kazi yao.
Amesema kwa
kuwa maofisa ugani hao wako kwenye Halmashauri zote wawasaidie wakulima namna
ya kupata mitaji kwenye taasisi za kifedha ili waweze kuzungumza lugha moja kwa
kuwafikia wakulima, wafugaji na wavuvi.
Kwa upande
wake waziri wa kilimo Hussein Bashe amesema viwanja vya maonyesho ya wakulima
vimefanyiwa ukarabati mkubwa ili kuwawezesha wakulima nchini kwenda kujifunza
kilimo bora kwa mwaka mzima.
Amesema kwa
sasa sekta ya kilimo imekuwa kutoka asilimia 2.7 hadi asilimia 4.2 mwaka huu wa
fedha huku lengo likiwa ni kufikisha asilimia 5 na ikifika mwaka 2030 sekta
hiyo ikue kwa asilimia 10.
Amesema kwa
sasa sekta ya kilimo ina uhakika wa soko na kwa mwaka huu serikali imefanikiwa
kuuza tani 600,000 za mahindi nchini Zambia.
Naye Mkuu wa
Mkoa wa Singida, Halima Dendegu amesema katika kukabiliana na mabadiliko ya
tabia nchi mkoa huo umeendelea kuwahamasisha wananchi kutunza mazingira ambapo
kwa kupitia miradi mkubwa ya umwagiliaji
yenye thamani ya Sh54 bilioni imeongeza eneo la umwagiliaji kutoka hekta
17 hadi hekta 21,400 sawa na asilimia 43 ya eneo lote linalofaa kwa
umwagiliaji.
Mwisho.


Comments
Post a Comment