KUTOKA KUOMBA OMBA HADI KUMILIKI DUKA LAKE

Muhtasari: Mwanamke huyo ambaye ni mlemavu wa viungo kwa sasa anamiliki duka ambalo limemsaidia kuachana na kuomba msaada kwa watu na sasa anaihudumia familia yake ya watu wanne kutokana na biashara hiyo ya duka.

Na Mwandishi Wetu, Chamwino.

MKAZI wa Kijiji cha Majeleko kilichopo Wilayani Chamwino Mkoani Dodoma, Melea Obed ambaye ni mlemavu wa viungo amejikuta akiachana na kazi ya kuomba misaada kwa watu baada ya kupata ufadhili wa kufunguliwa duka la kuuza mahitaji ya nyumbani.

Akizungumza na Kirimbo Blog leo jumatano, Julai 2024 Melea ambaye hawezi kukaa wala kutembea kutokana na ulemavu alionao amesema kabla ya kufunguliwa biashara ya duka alikuwa anashinda ndani  hata miezi minne bila kutoka nje.



Picha ikionyesha duka lililojengwa na mbao ambalo linamilikiwa na mlemavu wa viungo Melea Obed aliyekaa kwenye kiti mwendo.. Anayemwendesha ni Latwifa Saninga kutoka Shirika la Brac Maendeleo


Amesema hiyo inatokana na kutokuwa na uwezo wa kufanya shughuli yoyote kwa kuwa hawezi kushika kitu wala kutembea kwa miguu yake hivyo alikuwa anategemea wamtoe nje na kumrudisha ndani na alipokosa wa kumtoa nje alikuwa anakaa ndani bila kutoka nje hata miezi minne mfululizo.

“Nimekuwa hivyo kwa miaka 14, mimi nilikuwa ni wa kushinda ndani tuu hata mikutano ya kijiji nilikuwa siwezi kwenda nasubiri waliokwenda huko warudi waje wanihadithie yaliyozungumzwa huko, maana nilikuwa nasikia tu matangazo ya mikutano lakini uwezo wa kwenda huko nilikuwa sina,” amesema Melea.

Mwanamke huyo mwenye watoto wawili amesema hali ya maisha ilikuwa mbaya kwani watoto wake walikuwa wakiishiwa kalamu au madaftari walikuwa wakiomba kwa wasamaria wema ili wawasaidie kwa kuwa hakuwa na uwezo wa kuwahudumia.

“Hata maisha yangu yote yalikuwa ni ya kuomba kwa sababu siwezi kufanya kazi yoyote hali iliyosababisha mwanangu mkubwa kubeba ujauzito wakati anatutafutia chakula na hata aliyempa ujauzito huo hajulikani,” amesema Melea.

Melea amesema maisha yake yalianza kubadilika baada ya watu wa shirika lisilo la kiserikali la Brac Maendeleo Tanzania kufika kijijini hapo kwa ajili ya kuwasaidia watu wenye ulemavu na wanaoishi kwenye umaskini uliokithiri.

Amesema wakati wakiwatafuta watu wa aina hiyo ili wawasaidie ndipo na yeye alipokutanishwa nao na kutokana na hali aliyokuwa nayo walimtengenezea kiti mwendo ili aweze kukitumia kutembea kwenye maeneo mbalimbali badala ya kushinda ndani amelala.



Melea Obed ambaye ni mlemavu wa viungo akisaidiwa kuendeshwa kwenye kiti mwendo na Ofisa miradi kutoka Shirika la Brac Maendeleo Tanzania, James Komba


Amesema baada ya kupewa mafunzo ya kuwezeshwa kiuchumi alichagua mradi wa kuuza duka na kufuga bata ambao umebadilisha maisha yake kwani hivi sasa anahudumia familia yake kwa kile anachokipata kwenye biashara zake na ameachana na kuombaomba ili aishi.

Amesema anasaidiana na binti yake kwenye biashara hiyo huku kiti mwendo alichopewa kikimsaidia kuzunguka maeneo mbalimbali kwa ajili ya kutafuta bidhaa za kuweka dukani kwake badala ya kukaa na kusubiri kuletewa mzigo bila kujua thamani yake.

Amesema biashara hiyo imemsaidia kuishi yeye na mabinti zake wawili ambapo mmoja ni mwanafunzi wa shule ya sekondari pamoja na mjukuu wake mmoja.

Mbali na hilo amesema pia amejiunga kwenye vikoba ambapo wenzake walimchagua kuwa mwenyekiti wao mahali ambapo wanaweza kukopa na kuongeza mitaji kwenye biashara zao.

Melea amesema kwa sasa anahitaji jengo analolitumia kama duka  lenye ulinzi zaidi kwani alilonalo kwa sasa analazimika kuingiza bidhaa ndani baada ya muda wa kuuza kuisha na yeye hana nguvu za kubeba kutokana na ulemavu alionao na hata watoto wake bado wadogo hawawezi kubeba mizigo mizito kama mifuko ya sukari na unga.

“Natamani ningepata jengo imara ambalo nitakuwa nafungia bidhaa ndani kwa sababu hili la sasa haliko imara kwa sababu limejengwa kwa mbao hivyo inakuwa rahisi mtu kuvunja na kuiba….lakini pia ningepata umeme wa uhakika ambao utanisaidia kuuza mpaka usiku kwa sababu kwa sasa natumia tochi ambayo haina mwanga wa kutosha,” amesema Melea.

Mtendaji wa kijiji cha Majeleko Lidya Makasi amesema ni kweli wanatambua changamoto anazokutana nazo Melea katika kuboresha biashara zake lakini wanashindwa kuboresha mazingira kwa sababu nyumba anayoishi siyo ya kwake bali kuna msamaria mwema amempa aishi hapo.

“Hatuwezi kufanya maboresho ikiwemo kuvuta umeme au kujenga jengo la kudumu kwenye nyumba ya mtu bila ridhaa yake na ndiyo maana hata baada ya kupata ufadhili wa kufunguliwa biashara tulijenga duka la mbao ambalo muda wowote linaweza kuondolewa kama mwenye nyumba atahitaji tufanye hivyo.” Amesema Lidya

Kwa upande wake Mratibu wa mradi wa kuwajengea uwezo watu wanaoishi kwenye kaya maskini na wenye ulemavu (DIG), James Komba amesema Melea ni mmoja wa watu walionufaika na mradi huo kwenye kundi la watu wenye ulemavu.

Amesema mradi huo uko kwenye kaya 300 ambazo zinaongozwa na wanawake pekee pamoja na watu wenye ulemavu lengo likiwa ni kuwainua kiuchumi na kuondokana na hali ya utegemezi kutoka kwa ndugu jamaa na marafiki.

Komba amesema wanufaika wa mradi huo wamepewa mafunzo  na kujengewa uwezo wa miradi mbalimbali ya kiuchumi ikiwemo kufungua maduka, kilimo, ufugaji wa mbuzi, ng’ombe na nguruwe  ambapo shirika hilo limewawezesha wanufaika kwa kuwapatia wanyama wa kufuga pamoja na mitaji ya kufungulia biashara zao.

“Baada ya kuwapa mitaji na shughuli za kichumi hatujawaacha hivi hivi tumewakabidhi wa walimu wetu ambao watawasimamia na kuwakagua kila mara lakini pia tumewakabidhi kwa mabwana mifugo wa Halmashauri ambao watawapatia wanyama chanjo mbalimbali na hata kuwatibu pale wanapoumwa lengo ni kuwawezesha wajitegemee na kuachana na utegemezi waliokuwa nao,” amesema Komba.

Mwisho

 

 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

CHODAWU YAITAKA SERIKALI KURIDHIA MKATABA NAMBA 189 WA WAFANYAKAZI WA MAJUMBANI

NGOs ZAPEWA MWONGOZO WA KULIPA KODI NA TRA

TMDA YATOA MSAADA WA DAWA NA VIFAA TIBA VYENYE THAMANI YA SH 24 MILIONI