WACHIMBAJI WADOGO WATAKIWA KUTUMIA TEKNOLOJIA ZA KISASA KUCHENJUA MADINI BADALA YA KUTUMIA KEMIKALI YA ZEBAKI

 

Muhtasari: Wachimbaji wadogo wa madini nchini  wametakiwa kuzingatia matumizi sahihi ya kemikali ya zebaki inayotumika kwenye uchenjuaji wa madini ili kulinda afya zao na madhara yatokanayo na matumizi mabaya ya kemikali hiyo ikiwemo magonjwa ya ngozi, figo, kifua na hata kifo.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

WACHIMBAJI wadogo wa madini nchini wametakiwa kuzingatia matumizi sahihi ya kemikali ya zebaki inayotumika kuchenjulia madini ili wajiepushe na madhara yanayotokana na matumizi holela ya kemikali hiyo ikiwemo magonjwa ya ngozi, figo, saratani, kifua na hata kifo.

Ushauri huo umetolewa leo jumamosi Juni 22, 2024 na Baraza la Taifa la usimamizi wa mazingira (NEMC) na Ofisi ya  Mamlaka ya maabara ya mkemia mkuu wa serikali wakati wakitoa semina ya matumizi sahihi ya kemikali ya zebaki kwa wachimbaji wadogo wa madini nchini waliokutana Jijini Dodoma.

Akizungumza kwenye mafunzo hayo Mratibu wa Mradi wa Kudhibiti Matumizi ya Zebaki kwa Wachimbaji Wadogo  (EHPMP), Dk Betrina Igulu amesema wachimbaji wadogo wengi hawana uelewa wa madhara ya kemikali ya Zebaki na ndiyo maana wengi wao wameathirika na matumizi ya kemikali hiyo bila kujua.

Amesema wengi wao wanatumia kemikali hiyo bila kuchukua tahadhari zozote za kiusalama kama vile kuvaa mavazi yanayowakinga kugusana na kemikali hiyo, kuvaa glove mikononi, barakoa na mabuti na hivyo kujikuta wanaathirika na kemikali hiyo baada ya kipindi cha muda mrefu.


Mratibu wa mradi wa Mradi wa Kudhibiti Matumizi ya Zebaki kwa Wachimbaji Wadogo  (EHPMP),  kutoka baraza la taifa la usimamizi wa mazingira (NEMC) Dk Betrina Igulu




“Serikali haijapiga marufuku matumizi ya zebaki kwenye migodi lakini inatakiwa itumike kwa tahadhari kubwa na kwa kiwango kidogo ili isilete madhara kwenye afya zenu, kwa sababu unaweza ukadhani kuwa unatafuta fedha lakini hata ukiipata usiitumie kwa raha kwa sababu unakuwa na magonjwa yanayotokana na kemikali hiyo,” amesema Dk Igulu na kuongeza kuwa,

“Pia mnatakiwa kutumia zebaki kulingana na kiwango kilichoidhinishwa na shirika la afya duniani cha asilimia 15 tu kwani tulifanya utafiti kwa kushirikiana na Wizara ya afya kwa wachimbaji wadogo wa Mikoa ya Geita, Shinyanga, Mara, Mbeya na Singida ambapo tuligundua kuna matumizi makubwa ya kemikali ya zebaki hadi asilimia 60 na baadhi ya watu wameshapata magonjwa yanayotokana na kemikali hiyo.”

Amesema Nemc ina wajibu wa kulinda sheria ya mazingira ili kuhakikisha kuwa hakuna uharibifu wowote unaotokana na matumizi ya kemikali kwenye migodi ya wachimbaji wadogo na kwamba atakayebainika kuvunja sheria atafutiwa leseni yake ya uchimbaji.

Amewataka wachimbaji hao kuhifadhi kwa usalama mabwawa yanayohifadhi maji yenye kemikali ili yasilete madhara kwenye mazingira na kwenye vyanzo vya maji kwani ni hatari kwa viumbe hai.

Kwa upande wake Meneja wa kanda ya kati kutoka Ofisi ya mamlaka ya maabara ya mkemia mkuu wa serikali, Gerald Mollel amewataka wachimbaji hao kuhifadhi na kutumia kwa usahihi kemikali zote zinazotumika migodini.

Aidha amesema matumizi mabaya ya kemikali hizo ni hatari kwa afya zao kwani madhara hayataonekana haraka lakini baada ya miaka 10 ndipo yatakapoanza kuonekana ikiwemo kutetemeka mikono, miguu na kichwa, ngozi kubabuka, saratani na hata kifo.

Amesema hata kama wanatafuta fedha lakini wachukue tahadhari ya kulinda afya zao ili fedha watakazozipata waweze kuzitumia kwenye malengo waliyoyakusudia badala ya kutumika kujiuguza.

“Kuna kemikali nyingine hazihitaji kugusa moto hivyo unapozitumia ni lazima usivute sigara kwani kwa kufanya hivyo utaweza kutengeneza bomu ambalo litawaathiri watu wengi bila wewe kujua hivyo kabla ya kutumia kemikali hakikisha unasoma maelekezo ya matumizi yake na namna bora ya kuzihifadhi ili zisilete madhara,” amesema Mollel



Baadhi ya wachimbaji wadogo wa madini wakiwa kwenye mafunzo ya madhara ya kemikali ya zebaki Jijini Dodoma


Baadhi ya wachimbaji hao wameiomba serikali kuwaletea teknolojia mbadala ya kuchenjua madini yao badala ya kemikali ya zebaki kwani hata wakiitumia wanapata asilimia 55 tu madini wanayoyataka badala ya kuyapata yote.

Martha Mwageni amesema kama kemikali zinazotumika kwenye migodi zina madhara wanaomba serikali iwapelekee mitambo yenye teknolojia ya kisasa itakayowawezesha kuboresha kazi zao badala ya kuhatarisha afya zao kwa kutumia kemikali zenye sumu.

Amesema wachimbaji wengi wadogo wanatumia kemikali ya zebaki kwa kuwa ni rahisi kupatikana na kwa gharama nafuu bila kujali athari za kiafya zitakazowapata.

Naye Dk Mzeru Nibuka amewataka wamiliki wa migodi kuweka sheria ya kuwazuia watu waliolewa kufanya kazi kwenye migodi yao kwani huwa hawachukui tahadhari zozote za kiafya.

Amesema kama mtu anataka kulewa alewe baada ya kazi na si wakati wa kazi kwani hao ndiyo huwa hawavai vitendea kazi vya kuwakinga na kemikali za zebaki na mwisho wa siku ndiyo huwa wanaumwa na kuumia zaidi huko migodini wakati ndiyo nguvu kazi inayotegemewa.

Mwisho.

 

 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

CHODAWU YAITAKA SERIKALI KURIDHIA MKATABA NAMBA 189 WA WAFANYAKAZI WA MAJUMBANI

NGOs ZAPEWA MWONGOZO WA KULIPA KODI NA TRA

TMDA YATOA MSAADA WA DAWA NA VIFAA TIBA VYENYE THAMANI YA SH 24 MILIONI